Friday, April 23, 2010

“Ardhi ya nchi ndio mali yetu, wenzetu hawa wana matatizo ya ardhi, serikali itambue ardhi hii ni kwa ajili ya Watanzania, hivyo serikali ikafanye tafiti mipakani na kama kuna ardhi imeshanunuliwa kinyemela na wenzetu hawa irudishwe,”


- Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela (CCM)


Pengine kuna kila sababu ya kuhofu. Tanzania ina ardhi kubwa yenye rutuba. Ina zaidi ya hekta milioni 44 za ardhi inayofaa kwa kilimo, na ni robo tu ya ardhi hiyo, kiasi cha hekta milioni 10.5 ambayo inatumika kwa kilimo.


Japo naafiki maneno ya Mheshimiwa hapo juu ila naona panahitajika nyongeza kwamba serikali pia idhibiti ardhi kwa ufanisi zaidi siyo tu kutokana na hofu za kuporwa na watu wa nchi jirani.


Mara nyingine ni vigumu kuielewa mantiki iliyo nyuma ya kuwashupalia majirani kuhusiana na ardhi ilhali wananchi wa kawaida wanaendelea kuhamishwa kwa nguvu au kunyang’anywa ardhi na wageni wa kutoka mbali pamoja Watanzania wenyewe.


Kwa mujibu wa habari hii kuna ununuzi wa kinyemela wa ardhi uliofanywa Rufiji. Wahadzabe pia wameondolewa kwenye ardhi yao na shirika la kitalii bila maelewano mazuri.


Halafu kuna nchi zisizokuwa na ardhi ya kulima lakini zenye fedha ambazo zinaendelea kupata mgao wa ardhi kwa madai kuwa watatufundisha jinsi ya kulima vizuri kama wao. Hata Wamisri wana mashamba ya mboga Tanzania kwa madai hayo hayo ya kutunufaisha kwa mbinu bora za kulima mboga.


Kadhalika makampuni ya kimataifa yanayozalisha mazao ya nishati kwa madai kuwa tutapata faida kama vile fursa za ajira, fursa za masoko kwa bidhaa na mazao, upatikanaji wa nishati vijijini na mijini, kukua kwa uchumi wa wananchi, kupungua kwa umasikini, na kupungua kwa wimbi la nguvu kazi kukimbilia mijini.


Wakati tunawakalikia majirani, baadhi ya viongozi na Watanzania wengine wenye nafasi wamekuwa wakichukua ardhi kwa hila.


Basi likisikika suala la shirikisho la Afrika Mashariki, kama ada miiba inatusimama kama nungunungu tayari kushambulia.


Hivi bila ya mchakato wa shirikisho, masuala ambayo tunaweza kuyashikia usukani na ambayo tunapaswa kuyadhibiti kama vile ardhi - au kuboresha elimu na mbinu au viwango vya kushika ajira, ama kuboresha biashara ya utalii - yataendelea kubaki yalivyo?

1 comments:

njonjo mfaume said...

I am doing research on blogs and I would like to send u few questions. Can u help? If you are willing please send me your email, because it is not shown in your blog. My email is "njonjo.kweja@gmail.com" I am njonjo mfaume, tutorial assistant at School of Journalism of the University of Dar es Salaam, and MA Journalism student at Makerere University.